SOL CAMPBELL KUCHEKI MECHI YA NGAO YA HISANI TANZANIA

Kuna watu walipata nafasi ya kutimiza ndoto zao za kukutana na mastaa mbalimbali wanaocheza EPL, ikiwa ni ligi inayotazamwa zaidi Ulimwenguni na hata kupata nafasi ya kupiga nao picha huku Rooney akiwa ndio kivutio kikubwa huku haya yote yakiwezeshwa kwa udhamini mkubwa wa SportPesa.

Wakati mang’amung’amu hayo ya ujio wa Everton yakiwa bado vichwani mwa mashabiki wa soka, tayari kuna taarifa ya ujio mwingine mkubwa nchini kwa udhamini wa SportPesa.


Ikiutumia vyema ushirika wake na vilabu vya EPL, SportPesa sasa inamleta nguli na balozi wa klabu ya Arsenal kutoka jijini London ambao ni mabingwa mara 13 wa Ligi Kuu ya Uingereza huku pia wakiwa ni mabingwa wa kihistoria wa kombe la FA ambao wamelitwaa mara 13.

Mwaka 2001 alijiunga na miamba hiyo ya London akitokea Tottenham Hotspurs, Moja ya Mafanikio anayojivunia ni kuisaidia Klabu yake ya Arsenal kuweza kucheza michezo 49 bila kupoteza hata mchezo mmoja, ulikuwa ni msimu wa 2003/04 na kutwaa ubingwa wa ligi kwa staili ya aina yake kabisa. Huyu si mwingine bali ni Sol Campbell


Alifanikiwa Kucheza michezo 200 akiwa na Arsenal na kufunga magoli 12, tulizoea kumuona kwenye runinga akisakata kabumbu safi na la kibabe haswaa, pia alipostaafu bado tulimuona akiuchambua mpira kwa ustadi wa hali ya juu.


Kupitia kampuni ya mchezo wa kubashiri ya SportPesa, wamefanikiwa kumleta Gwiji huyo Tanzania. Sol Campbell anatarajia kutua katika ardhi ya Tanzania na kufungua njia ya mahusiano mazuri ya kimichezo kati ya Tanzania na Klabu Ya Arsenal kupitia SportPesa ambao ni washirika rasmi wa Arsenal katika michezo ya kubashiri kwa bara la Afrika.



Arsenal na SportPesa waliingia mkataba wa miaka mitatu na nusu ambao utaishuhudia klabu hiyo ya Arsenal ikileta maofisa wake wa benchi la ufundi kwa ajili ya kuendesha kliniki za soka kwa makocha na wachezaji barani Afrika na tayari wameshafanya hivyo mara kadhaa nchini Kenya.

Atakapokuwa nchini, Sol Campbell atapata nafasi ya kutembelea klabu ya michezo ya walemavu ya Muungano na kubadilishana nao mawazo na kisha siku ya tarehe sita pia atatembelea shule ya soka ya Magnet katika viwanja vya Gymkhana ambapo atapata nafasi ya kukutana na wachezaji chipukizi, kucheza nao na pia kuwapa hamasa katika safari yao ya soka.

Kubwa zaidi ni pale ambapo Campbell ataongoza jopo la wapenzi wa klabu ya Arsenal nchini kutazama mechi ya Ngao ya Hisani siku ya Jumapili ya Agosti 6 kati ya klabu ya Arsenal ambao ni mabingwa wa FA dhidi ya Chelsea ambao ni mabingwa wa EPL.
Hakika itakuwa ni fursa adhimu kwa wapenzi wa mpira nchini hususani wale wa Arsenal kukutana na nyota wao huyo wa zamani, kuongea na kupiga nae picha ikiwa ni ndoto ya kila shabiki wa soka duniani kukutana na nyota anayemkubali.

Ikumbukwe kuwa Arsenal ni klabu inayoongoza kwa kuwa na mashabiki wengi nchini Tanzania hali kadhalika barani Afrika. Hivyo naona jinsi ambavyo ujio huu wa Sol Campbell unavyotimiza ndoto za kundi kubwa la mashabiki wa soka nchini. Upo tayari?

No comments

Powered by Blogger.