KWAHERI ADEN RAGE,KAMA TUKISAHAU TUTAKURUDISHA TENA KWA MATARUMBETA


 
                 Binadamu tumeumbwa kusahau Yani utashangaa Leo tunalia ,kesho ikifika tunacheka kidogo tunasahau kilio cha jana. Ndivyo tulivyoumbwa wanadamu,ndivo tulivyo  Waafrika,Wazungu na Waarabu pia. Umeshajiuliuza tusingeumbwa kusahau ingekuaje? Labda  tusingeumbwa kusahau tungeumbiwa roho za chuki na visasi mioyoni mwetu.Labda tusingeumbwa kusahau tungejikinga na vitu vilivyotuletea simanzi jana ili tusipate huzuni tena kesho.sijui jibu sahihi ni lipi kwako Mtanzania. Mtanzania wewe wanaekulaghai kwa miezi 6 ili uwe mtumwa wa miezi 54,hii yote haya kwasababu umeumbwa kusahau.

                 Watanzania tumekuwa wagumu kubadilika kwasababu ya usahaulifu wetu. Leo hii  mtanzania atalalamika kwa kukosa huduma za msingi za kijamii ambazo mwakilishi wake alimuahidi atampatia pindi tu atakapomchagua,lakini mwakilishi huyo huyo aliyeshindwa kutimiza ahadi zake ipo siku atarudi tena kwa mtanzania huyo huyo na kumuomba kura huku akimuadaha na maneno laini yanayosindikizwa na kanga,kitenge,kofia  na shilingi elfu kumi,Hapo hapo mtanzania huyo atasahau nini alikihitaji kutoka kwa kiongozi huyo,atasahau shida zote alizozipata kwa miaka mingi na atauza kura yake kwa shilingi elfu kumi ya siku moja bila kujali shida atazozipata kwa siku zaidi ya elfu moja.Huyo ndio mtanzania.Ndio maana kila siku viongozi wetu ni wale wale na sisi tupo vile vile hakuna  mabadiliko.

                  Mwezi wa tano mwaka 2010 timu ya simba ilifanya uchaguzi katika ukumbi wa bwalo la polisi oysterbay  uliomuweka Aden rage kua mwenyekiti wa simba kurithi nafasi ya Hassan dalali aliyemaliza muda wake, huku ndugu kaburu akichaguliwa kua makamu mwenyekiti .Kabla ya hapo Aden rage aliwai kua makamu mwenyekiti wa FAT pia katibu mkuu wa taasisi hiyo.Kwa ufupi aden rage hakuna kipya alichofanya FAT.Lakini rage huyo huyo aliweza kurudi tena na kuwashawishi wanasimba na kumpa  ushindi wa kishindo.Rage huyo huyo ndio aliyeongoza FAT iliyodumaa walimsindikiza kwa nderemo na vifijo kuchukua fomu.Rage huyo huyo aliyefungwa kwa ubadhilifu wa mali za fat ndio huyo huyo wakampa dhamana ya kulinda mali za simba. Ama kweli binadamu tumeumbwa kusahau.Ila kama kusahau ni ugonjwa watanzania tunakaribia kufa.

                    Siku chache zijazo Simba itaingia kwenye uchaguzi  mkuu.Tumeona watu wanasindikizwa kuchukua fomu za kugombea uongozi  wakisindikizwa na mavuvuzela.Ukipita kwenye matawi  huko ndo usiseme.Watu wamecharuka,kila mtu na mgombea wake.Hivi ndivyo kampeni inavyokuwa. Nderemo vifijo na shamrashamra kutoka kwa wagombea. Ila wapiga kura hao hao wengi wao baada ya kupiga kura hujutia maamuzi yao.Hutamani siku zirudi nyuma watoe shilingi kwa waliowapa kura zao.Lakini wakati uchaguzi ukifika tena hufanya makosa yale yale ya kupiga kura kwa watu ambao si sahihi.

                Zipo sababu nyingi zinazosababisha watu kutofanya maamuzi sahii katika uchaguzi wa viongozi.Lakini hizi ni sababu kuu zinazopelekea watu haswa wanachama wa vilabu vyetu vikongwe kung’ata vidole vyao wenyewe wakati wa kupiga kura.

                   Kwanza ni kufuata mkumbo,wapiga kura wengi haswa watanzania wanapiga kura kwa kufuata mkumbo.Wapiga kura wengi ni wavivu wa kusikiliza na kuchambua sera makini za wagombea.Wapiga kura wengi wanakosa taarifa muhimu za wagombea.Wapiga kura wengi wanaamini kwenye maneno ya umbea,vijembe na majungu.Wengi wao wanapiga kura kwasababu ya fulani kasema huyu anafaa na yule hafai.Ila ukimuuliza kwanini anafaa? au kwanini hafai? hasilani hatakupa jibu sahihi.Kama mpiga kura inabidi usiwe mtu wa mkumbo.inabidi ufanye upembuzi yakinifu kwa mgombea unayetaka kumpa dhamana ya kukuongoza.Inabidi ujue kwanza alifanya nini bila kusahau anataka kufanya nini na hiko anachotaka kufanya atakifanyaje?.Mpiga kura mwenye hekima ataachana na stori za vijiweni na kutazama vitu hivi.

                       Imani potofu ya mpira pesa,Siku hizi kuna maono mapya ya dunia. Ndani ya maono  hayo kuna bosi mmoja tu. Bosi huyo ni pesa.Miaka ya nyuma ili uheshimike kwenye jamii ilikua lazima uwe na Elimu,Hapo utashinda dhidi ya umma. Maono mapya ya Dunia yanaamini mtu mwenye busara,Hekima na kustahili  Kuheshimiwa ni yule mwenye pesa.uwe mwandisi,daktari,mwalimu bila shekeli hakuna atakayetambua na kuthamini wala kuheshimu taaluma yako.

                     Kwenye Dunia yetu mpya watu wameweka pesa mbele.Kinachonifurahisha zaidi hata kwenye ulimwengu wetu wa soka pesa ndiyo inacheza mpira lakini watu wamesahau pesa hiyo hiyo ndio inaharibu mpira.

                        Pesa si kila kitu kwenye soka.”Heri masikini mwenye hekima kuliko tajiri mpumbavu”.Watu wengi wenye pesa hupenda kuongoza timu kwa manufaa yao wenyewe.Ndio maana wengi wao huzunguka mbuyu ili kuukwaa uongozi.Watu wengi wenye pesa huwa na malengo ya kuongeza pesa zao kulilko kuitumikia timu.

                      Simba  tangu ianzishwe imeongozwa na watu wenye pesa wangapi? Na watu hao wenye pesa wameifanyia nini cha ziada wakati wa uongozi wao zaidi ya kutunisha matumbo yao na kujiongezea umaarufu?

                        Wanachama wa simba msiende mbali,muangalieni mtoto wa mama yenu wa kambo.Tangu mtoto wa mama yenu wa kambo aongozwe na yule tajiri mwenye asili ya ki Asia  wamepiga hatua gani ya ziada? Ndio wale wale jana na leo na hata kesho watabaki vile vile japokua wamekubali kumuongezea mwaka mmoja zaidi,lakini hakuna cha ziada atakachokifanya.Ahadi nyingi kubwa aliahidi mpaka sasa hajatekeleza.

                         Najua mna mtihani wa kuchagua kiongozi bora kwasababu viongozi wengi ni wale wale wa mwaka jana na juzi,lakini kama hayupo bora basi atakuwepo kiongozi sahihi wa kuiongoza simba kwa miaka minne ijayo.Nnachowasihi wanachama wa simba waache kufuata  mkumbo,shirikisha ubongo wako.Usiuze kura yako wala kuchagua kiongozi kwasababu ya pesa yake ambayo wewe hautakua na faida nayo.Busara na hekima ndio sifa za kiongozi sahihi atakayewavusha salama miaka hii minne.

                       
                                     By

                                     Allen kaijage a.k.a middle ya juu

                                      kaijagejr@gmail.com

                                       0655106767
++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++

No comments

Powered by Blogger.