ARSENE WENGER ~ MSEMINARI WA KALE ANAYEHUBIRI INJILI KWENYE SOKA


Katika maisha yangu sijawahi ona watu wenye imani kali kama wahubiri wa dini, Mapadri ,masheikh na wachungaji hawa watu wana imani kali sana na dini zao. Imani zao zimejengwa kwa kusoma na kusikia mafundisho ya vitabu vitakatifu.
Vitabu Vitakatifu Vinatuambia “Imani huja kwa kusikia ,tena kwa kusikia neno la Mungu” na Ili Shekh uitwe Shekh lazima uwe una Imani thabiti ya dini ya kiislamu ilojengwa kwa misingi ya kurani. Na mchungaji vivyo hivyo,Lazima awe amejazwa neno la Imani kupitia misingi thabiti ya biblia.
Lakini hakuna shekh aliekua shekh bila kupitia Mafundisho thabiti ya Dini ya kiislam,na ili uwe padre lazima upitie Seminari. Achana na Seminari magamaga za siku hizi Kila mtu akijenga shule anaiita seminari. Matokeo yake wanatuzalishia "magigisi" na "magobo"
Seminari zilikua zamani bwana,Mtu akitoka seminari hata bila kukwambia utamjua tu. Tabia hata hekima yake itaongea tu. Wachungaji na Mapadre waliosoma seminari za Kale walifundwa wakafundika, walikanywa wakakanyika. Hawa watu ni ngumu kuwatenganisha mbali na imani zao.
Hawa watu huwezi kuwabadilisha kwenye kile wanachokiamini. Mchungaji na padre walishafundishwa,wakasikia pia wakasoma kua Isaka ni mzaliwa wa kwanza halali wa Ibrahim.Hasilani huwezi kumbadilisha na kumwambia Ismail ndie mzaliwa wa kwanza halali wa Ibrahim.
Kesha ukeshavyo, Huubiri uhubirivyo hawezi kubadili msimamo wa watu hao watu asilani. Mpige mawe kama Stephano, muwekee kisu shingoni bado atachukua mbundugo na kuendelea na Imani yake. Mchungaji anaamini akimuombea kiwete atatembea tena,akimuombea kipofu ataona tena,kiziwi pia atasikia tena.Muda mwingine kipofu huwa aamini kua siku moja akiombewa ataona,ila mchungaji ana imani asilimia zote kua kipofu lazima atapokea uponyaji.
Hata akimuombea mara ya kwanza kipofu asione ila bado atakua na imani ipo siku kipofu huyo ataona tena kwakua alishawai ombea vipofu wengine wakaona tena. Huo ndo ujasiri wa mchungaji,hiyo ndo imani ya mchungaji.
October 22, Mwaka 1949 mjini Strasbourg alizaliwa muinjilisti wa soka, Mwenye imani kali kama Ibrahim.Huyu ni mtoto wa mzee Alphonce,aliyekua mfanya biashara maarufu wa vipuri mjini Strasbourg.Alitumia muda mwingi kuangalia mpira akiwa bar.Hakika soka ilikua ndani ya damu yake.Alitumia mbinu alizoziona bar na kuziamishia kwenye timu yake ya kijiji.
Tangu kijana alipenda kazi ya ukocha kuliko kucheza mpira.Mda mwingi alikua akipanga kikosi kwenye timu yake ya kijiji amayo baba yake alikua akifundisha.Maisha yake ya soka kama mchezaji yalianzia kwenye timu ya kijiji cha Duttlenheim,kijiji ambacho alikulia mseminari huyu.
Hakuna aliyemjua muinjilisti huyu kwenye maisha yake ya uchezaji. Alitundika daruga akiwa na timu ya RC Strasbourg na kufungua ukurasa mpya katika ngazi ya ukocha. Maisha yake kama kocha yalianza mwaka 1981 mara alipohitimu shahada yake ya biashara na kukabidhiwa mikoba kama kocha wa timu ya vijana katika timu ya RC Strasbourg. Mwaka 1983 akateuliwa kua kocha wa vijana wa timu ya cannes kabla ya kutimkia katika klabu ya Nancy Lorraine mwaka mmoja baadae,mwaka 1987 klabu ya Nancy ikashuka daraja.

Wengi walifikiri huo ndo utakua mwisho wa mseminari huyu katika maisha yake kama kocha La hasha huo ndo ulikua mwanzo wa nyota yake kuangaza. Mnamo mwaka 1987 klabu ya Monaco ikampa ajira ya kua kocha wa timu hiyo,uteuzi huo ulileta maswali mengi sana,hakuna aliyeamini klabu kubwa kama Monaco itamteua kocha alioyeishusha timu daraja.”Hakika huyu ni mwana wa Mungu”,ni mmoja wa watu wenye bahati katika sayari yetu. Msimu wake wa kwanza akiwa na Monaco akaiwezesha klabu hiyo kuwa bingwa wa ligi kuu ya ufaransa,pia mwaka 1991 aliiwezesha Monaco kua bingwa wa kombe la ufaransa.
Katika kipindi chake kama kocha wa Monaco alipata kuwasajili wachezaji kama Glenn Hoddle na George Weah ambae baadhi ya watu walikejeli usajili wake lakini mwamba huyo wa Afrika miaka kadhaa mbele ukaibuka kua mchezaji pekee bora duniani kuwahi kutokea kwenye Dunia yetu ya tatu.
Huo ndo ujasiri wa mseminari huyu ulipoanzia. Mwaka 1994 alishindwa kukubaliana na uongozi kuhusu mkataba wake na klabu ya Monaco. Kumbuka klabu ya Monaco ilimzuia kwenda kufundisha katika klabu ya Bayern Munich mwaka huo huo. Huo ndo ulikua mwisho wake wa huduma kama kocha kwa klabu ya Monaco na Ufaransa kwa ujumla. Ailitimkia kwenye klabu ya Nagoya Grampus kabla ya kupigiwa pande na rafiki yake David Dein kuinoa klabu ya Arsenal mwaka 1996. Timu zote alizofundisha awali zilikua shule hapa ndipo alipoanza rasmi kazi yake ya uinjilisti.
Utamwambia nini huyu mtu akuelewe wakati washabiki wa Arsenal hawakumuelewa alipotumia pesa kumnunua Dennis Bergkamp. Wengi walilalamika pesa zilizotumiwa kumnunua mdachi huyo. Ni yeye pekee aliyeamini Begkamp ana thamani hiyo. Baadae kidogo Bergkamp akawaonesha mashabiki kuwa Wenger alikua sahihi kuliko wao.
Unamkumbuka Nikolas Anelka? Wakati anasajiliwa kinda huyu kila mtu alimnyooshea kidole. Magazeti yote yakamuadaa na kuona kama amefanya kituko cha usajili, Ila mzee huyu na imani kama ya Abrahamu akamuamini Anelka vivyo hivyo Anelka nae akampa kocha wake kile alichokiona kutoka kwake. Mashabiki na wadau wakabaki midomo wazi,huku vyombo vya habari vikiwa vimepigwa bao la pili na mfaransa huyu.
Robbin van Persie aliandamwa na majeruhi,mashabiki wengi sana walipendekeza auzwe hasa pale Juventus walipotuma ofa. Lakini muinjilisti huyu akamkumbatia kilema wake huku akiamini ipo siku kilema wake atatembea tena. Aliamini ipo siku RVP atakua gumzo katika ligi ya uingereza na ndivyo ilivyotokea ,washabiki walotaka auzwe wakasahau wakaanza kumshangilia.
Aaron ramsey,huyu mpiganaji wa kiingereza, wenyewe humuita Rambow, ni mchezaji bora wa arsenal mwaka 2013,licha ya kupata majeruhi bado anatarajiwa kua mchezaji bora wa arsenal mwaka 2014. Huyu ni muingereza haswa,hujitoa asilimia mia ndani ya uwanja,hutoa kila kitu kwa ajili ya timu yake. Kila mshabiki wa arsenal anampenda Rambow,ila bila imani ya kocha wake huyu Ramsey asingekuwa mchezaji wa arsenal kwa sasa.
Huyu mtoto wa mzee Aliphonce ana imani kama ya David Oyedepo,aliamin ipo siku Ramsey atakua nyota.Lakini mashabiki wa arsenal waliona ramsey ni kama mgonjwa wa ukimwi,hawakuamini kama atapona siku moja.Ni yeye tu aliyemuamini

Lakini Huyu mzee wetu kuna mambo matatu ameamua kuyafumbia macho.Hayo ndo yalioifanya arsenal ikose ubingwa kwa miaka nane na huu unaenda mwaka wa tisa bado anafanya makosa yale yale yatakayomfanya atoke kappa tena.
Kosa la kwanza ni kufumbia macho nguvu ya pesa ya Chelsea na Manchester City. Bado anaiishi jana yake leo,Anaamini soka la karne ya 20 ni sawa na soka la karne hii. Katika utawala wake alikua akishindana na Manchester U nited pekee.Manchester United ikiteleza Arsenal ilikua haifanyi makosa.
Tangu utawala wa Chelsea na Man City uanze Arsenal wametwaa taji moja tu. Arsenal ya sasa inahitaji kutumia mabavu ya pesa ili kushindana na Chelsea na Manchester City. Huwezi kuchukua kombe wakati unawategemea Sanogo na Giroud na huku mwenzako ana Dzeko na Jovetic katika benchi la wachezaji wa akiba.

Pili ni Kuendelea kukumbatia wachezaji wasiompa matokeo.Tunajua kama wewe ni baba wa imani kwenye soka ila kwanini usijifunze kwa yaliyokupata awali. Richard Wright, Denilson,Andre Santos,Francis Jeffers,Igors Stepanovs,Sebastian Squillaci hawa ni miongoni wa wachezaji mizigo aliowaamini na kuwapa nafasi. Licha ya kuwaamini na kuwang'ang'ania bado hawakumpa matokeo,mwisho wa siku wachezaji hao wakaitia hasara klabu.Ila bado hajakoma tu,bado anaamini kwa Giroud. Akimuangalia Giroud anamuona Henry ndani yake,imani yake ndio inamuongoza hivo.

 

Kosa lake kubwa na la mwisho kushindwa kufanya mabadiliko na marekebisho kwa kila sekta katika timu kwa msimu.Kuna msimu Arsenal inakua na beki nzuri na viungo wazuri lakini inakosa mmaliziaji mzuri(mfano msimu huu),kuna msimu inakua na beki mbovu ila wanapata viungo wazuri na washambuliaji wazuri,pia kuna msimu wanakua na beki imara na washambuliaji maridadi lakini viungo wanarega.Wakati akiendelea kumsubiri RVP Cesc Fabregas alikua akiibeba timu licha ya kuongozwa na safu nyepesi ya ushambuliaji iliyokua ikiongozwa na Adebayor.Mungu si Athuman Robbin van Persie akarejea lakini msimu unaofuata tangu Rvp arejee akamuuza Cesc Fabregas.
Kiungo cha Arsenal kikalega,Akaanza kumuamini Ramsey huku Thomas Rocisky akirejea taratibu kuziba pengo la Fabregas kipindi hicho Rvp anaibeba timu, Lakini msimu unaofuata akamuuza RVP ambaye alikua mmoja wa washambuliaji hatari Duniani na kumnunua Olivier Giroud kama mbadala wake,mpaka wa leo Giroud viatu vya RVP havimtoshi.

Pata picha Arsenal ya leo ingekua na RVP na Samir Nasri,ungekua unahitaji nini kwenye Dunia ya soka.Arsenal ilikua inahitaji mtu kama suarez ili avae viatu vya RVP, keshokutwa atatafuta mshambuliaji mkali huku akisahau Rocisky na Cazorla umri unawatupa mkono. Huyu kila msimu anakomaa kuimarisha sekta moja au mbili tu.Kwake siku zinaganda,miaka haiendi.Huyu ndie Baba wa imani,mimi napenda kumuita muinjilisti,Huyu ndie ARSENE WENGER,mwenye roho ya kiseminari,imani ya kichungaji, hua akubali kupingwa kutoka kwenye kile anachokiamini, hua apangi kushindwa, ila anashindwa kupanga.

 

By Kaijage jr

Middle ya juu


No comments

Powered by Blogger.