MANE ATUMA ZAWADI YA JEZI ZA LIVERPOOL KIJIJINI KWAO

Mshambuliaji Sadio Mane ametuma jezi 300 za Liverpool kijijini kwao kwa ajili ya mashabiki kuvaa katika mchezo wa kesho wa fainali ya ligi ya mabingwa Ulaya kati yao na Real Madrid.

Nyota huyo alikuwa akiishi kijini kwao Banbali kusini mwa Senegal mwaka 2005 wakati Liverpool ikicheza fainali yake ya mwisho ya michuano hiyo dhidi ya AC Milan katika mji wa Istanbul, Uturuki.

Mane anakumbuka aliangalia mechi kwa njia ya Luninga ambayo Liverpool ilitoka nyuma kwa mabao matatu na kushinda kwa penati hivyo anaamini hata kesho wanakijiji watatazama fainali hiyo itakayopigwa mji wa Kiev nchini Ukraine.

"Kwangu ni furaha kubwa kucheza fainali ya michuano hii, ni matumaini yangu tutatwaa ubingwa. Familia yangu bado inaishi kijiji mama yangu na mjomba bado wapo kule na watatazama fainali.

"Kijijini kuna wakazi 2,000, nimewatumia jezi 300 za Liverpool kwa mashabiki kuvaa siku ya kesho. Nitaenda kuwasalimia majira ya joto baada ya fainali za kombe la dunia nikiwa na medali ya ubingwa wa Ulaya," alisema Mane.

Liverpool haipewi nafasi kubwa ya kuchukua ubingwa wa michuano huku Madrid ikitafuta taji hilo kwa mara ya tatu mfululizo.

No comments

Powered by Blogger.