BOCCO APIGA BAO ZOTE 2 SIMBA IKILA VYEMA KIPORO CHAKE NJOMBE

Vinara wa ligi kuu soka Tanzania bara wekundu wa Msimbazi Simba wamefanikiwa kushinda mechi yao ya kiporo dhidi ya Njombe Mji kwa bao 2-0 mchezo uliopigwa jioni hii katika uwanja wa Saba saba Mjini Njombe 

Shukrani za kipekee ni kwa nahodha John Bocco ambaye alifunga bao zote mbili katika mechi hiyo iliyochezwa katika Uwanja ambao ni mara ya kwanza kwa Simba kucheza 

Mpaka kipindi cha kwanza kinamalizika Simba tayari walikua mbele kwa bao 1-0 bao lililofungwa na John Bocco baada ya kupokea mpira mrefu wa beki yusuph Mlipili na kuutuliza vyema kisha kugeuka na kupiga shuti kali la mguu wa kulia na kuiandikia Simba bao la kwanza ikiwa ni dakika ya 16 ya mchezo 


Kipindi cha pili simba hawakuonekana kujali sana kuhusu kucheza mpira wa pasi nyingi bali waliangalia matokeo hasa kutokana na ubovu wa uwanja wa Sabasaba na John Bocco akawainua tena mashabiki wa simba kwa kufunga bao la pili akitumia vyema mpira wa Shomari Kapombe.


Haruna Niyonzima na Salim Mbonde ni kati ya wachezaji wa Simba waliorejea leo kikosini baada ya kukaa nje kwa muda mrefu kutokana na majeraha 


Kwa matokeo hayo Simba wanaendelea kukalia kiti cha uongozi wa ligi hiyo wakiwa na pointi 49 baada ya michezo 21 huku Yanga ambao ni mabingwa watetezi wakibaki katika nafasi ya pili na pointi zao 46

No comments

Powered by Blogger.