TAIFA STARS YAFIKA SALAMA, KUANZA NA MALAWI

Kikosi cha wachezaji 22 wa timu ya Tanzania ‘Taifa Stars’, kimesafiri na kufika salama nchini Afrika Kusini kikitokea Dar es Salaam, Tanzania.

Timu hiyo iliyoondoka Alhamisi Juni 22, 2017 kwenda Afrika Kusini kwa ndege ya Shirika la Ndege la Rwanda, itakuwa huko kwa ajili ya michuano ya kuwania Kombe la Castle Cosafa.

Taifa Stars inayodhaminiwa na Bia ya Serengeti, itaanza kampeni za kucheza hatua ya Robo fainali kwa kucheza na Malawi Jumapili, Juni 25, mwaka huu katika michuano hiyo iliyoandaliwa na Baraza la Mpira wa Miguu la nchi za Kusini mwa Afrika (Cosafa).

Tanzania si mwanachama wa Cosafa, lakini imealikwa katika mashindano hayo na imepangwa kundi A na timu za Mauritius, Malawi na Angola wakati Kundi B ni Msumbiji, Shelisheli, Madagascar na Zimbabwe. Kinara wa kila kundi atakwenda moja kwa moja hatua ya robo fainali.

Timu za Botswana, Zambia na Afrika Kusini kadhalika Namibia, Lesotho na Swaziland tayari zimepangwa hatua ya robo fainali hivyo zinasubiri vinara wawili kutoka makundi ya A na B kuungana nazo kucheza robo fainali.

Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Salum Shabani Mayanga, amesema kwamba anaichukulia michuano hiyo kwa umakini na uzito mkubwa kwa wachezaji kuzidi kupata uzoefu wa mechi nyingi za kimataifa kwa mwaka.

Kadhalika, kiufundi Mayanga anachukulia michuano hiyo kama sehemu ya maandalizi makubwa ya mchezo dhidi ya Rwanda wa kuwania kucheza nafasi ya kushiriki fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika kwa wachezaji wanaocheza ligi za ndani - CHAN.

No comments

Powered by Blogger.