KUNA CHA KUJIFUNZA CECAFA



NA ASHA MUHAJI
MWANAFUNZI shujaa haogopi kupiga chabo! Maisha pamoja na kufanikiwa ni lazima kujifunza. Kama unataka mafanikio basi huna budi kuiga kwa mtu anayefanya vizuri zaidi yako. Huo ndiyo ukweli wa mambo ulivyo.
Hali si nzuri sana katika soka la Tanzania na kila mdau amekuwa akitoa mawazo yake ili tu kuhakikisha mchezo unapiga hatua na kamafikio kupatikana.
‘Nani amfunge paka kengele’? Hakuna muda wa kusubiri kwani mengi yameshasemwa na bado kasi ya kufika katika nchi ya asali waliko wengine ni ndogo mno, hivyo kuchepua mwendo na kuongeza kasi ni lazima iwe isiwe.
Nchini Ethiopia kuna michuano ya ….. ya Kombe la Chalenji inaendelea ambapo kwa nchi kama Tanzania kuna kitu muhimu sana cha kujifunza kutoka kwa nchi zingine.
Katika michuano hiyo inayoshirikisha jumla ya timu za mataifa 12 ambapo 11 kati ya hizo ni kutoka ukanda huu wa Afrika Mashariki na Kati na moja iliyobakia Malawi ikishiriki kama timu mualikwa kutoka ukanda wa Cosafa (Kusini mwa Afrika).
Nchi zote hizo zinapishana sana kiwango lakini cha msingi kinachotakiw ani kila moja kujitathimini na kufahamu malengo yake ni nini kufika wazlikofanikiwa wengine.

Katika michuano hiyo nchi za Uganda ‘The Cranes’ na Rwanda ‘Amavubi’ zimepeleka vikosi vya wachezaji wengi vijana lengo likiwa kuitumia michuano hiyo kutengeneza vikosi vyao kwa ajili ya Michuano ya CHAN ambayo fainali zake zinatarajiwa kufanyika Januari mwakani nchini Rwanda.
Kuna tofauti kubwa za vikosi hasa kile cha Uganda kilichoshiriki mechi za mtoano kuwania kupangwa katika makundi kwa michuano ya Kombe la Dunia pamoja na hiki cha sasa kinachoshiriki Chalenji. Katika kikosi cha The Cranes wachezaji wengi ni vijana wenye umri chini ya miaka 23 isipokuwa wachache sana waliochomekewa ili kuiongezea nguvu timu hiyo. 
Kitendo cha nchi hizo kupeleka vikosi vya wachezaji wao wengi vijana ni dhahiri wanalenga mafanikio katika timu kwa kuwa hao watakuwa hazina kubwa kwa nchi zao miaka mchache ijayo. Hakika soka la vijana ndiyo suluhisho ya matatizo ya kisoka yanayoikabili Tanzania hivi sasa.
Mpango kama huo umetumiwa na Nigeria ambayo mwaka huu timu yake ya taifa ya Vijana wenye umri chini ya miaka 17 imetwaa ubingwa wa dunia na baada ya miaka miaka miwili au mitatu ijayo itakuwa na timu bora.
Bila shaka kikosi hicho kitafanya makubwa katika fainali za wakubwa za Kombe la Dunia zitakazofanyika mwaka 2020 nchini Qatar.
Nchi kama Senegal ilifanikiwa kuwa na timu bora ya taifa kutokana na msingi madhubuti waliouweka katika timu za vijana kupitia Bruno Metsu na akafanikiwa kuwazalisha kina Khalilou Fadiga ma El Hadji Diouf wengi sana.
Vilevile nchi kama Mali nayo ilifaidika sana na programu za timu za vijana na mwisho wa siku ikatengeneza wachezaji wengi sana tegemeo kwa kikosi chake cha wakubwa kama vile Seydou Keita.
Wadau wa soka wa Tanzania pamoja na taasisi zinazosimamia mchezo huo zinapaswa kujifunza kitu kutoka Michuano ya Chalenji hasa kuhusus uwekezaji wa soka la vijana.
Nchi nyingi zimekuwa zikiitumia michuano hii kuzitengeneza timu zao kwa ajili ya michuano mingine mikubwa kama ile ya AFCON na Kombe la Dunia.
Kulaumu Serikali hakuna tija tena kwani kila mdau ana nafasi yake. Kabla ya kuilamu Serikali tujiulize kila mdau kwa nafasi yake amefanya  nini?       
Lakini nini msaada wa klabu za Tanzania katika mchango huu ili kuleta mageuzi ya mchezo huu hapa nchini. Ikumbukwe Ligi Kuu ndiyo chimbuko la timu ya taifa, lakini je zina mkakati gani na timu za vijana? Nini mchango wake kuinua soka?
Klabu hazina malengo mazuri kwa soka la Tanzania kwani ziko kibiashara zaidi kuliko kuwa na mikakati ya kukuza kiwango na mchezo huo kwa ujumla na badala yake zimekuwa zikishindwa kupata faida kwakuwa kiwango kiko chini hivyo zinaishia kufanya vibaya tu.
Ni aibu kubwa sana kutumia mamilioni ya fedha lakini miaka nenda rudi kiwango bado kiko chini tu badala ya kukua eti kinaporomoka tu.
Nchi kama Uganda iliyokuwa inanyanyaswa na Tanzania kuanzia ngazi za klabu mpaka taifa leo hii imekuwa tishio kwa soka la nchini. Kilichowakomboa ni kujitathimini na kuweka malengo ambayo yamefanukiwa kupitia hazina ya uwekezaji wa soka la vijana.
Sasa ni wakati wa kuacha kuingiza siasa katika michezo hususani soka. Msingi wa kuwa na timu bora ya taifa siku zijazo ni kuwa na mfumo unaozalisha timu za vijana ambao kadri siku zinavyokwenda wanapata nafasi ya kupandishwa.
Kuna ubaya gani wa kujifunza? Si vibaya kwa Tanzania kujifunza kutoka kwa wengine hasa majirani zake wanaoonesha kila dalili ya kufanikiwa.   


No comments

Powered by Blogger.