LIGI KUU VPL 2015/16 KANYAGA TWENDE

Kipyenga cha Ligi Kuu ya Tanzania Bara ndiyo hicho kimelia sasa ni wakati wa kila timu kuonesha nini ilichopanda kuelekea msimu wa mavuno wa 2015/2016.
Kuanza kwa Ligi hiyo ni safari nyingine ndefu ya matumaini ya kumpata Bingwa wa Tanzania siyo tu atakaeng’ara kwa timu zingine 15 bali ndiye atakayekuwa mwakilishi wa nchi katika michuano ya kimataifa ambapo atashiriki Klabu Bingwa Afrika 2016.
Licha ya kushirikisha timu 16 msimu huu kuna kila dalili kuwa msimu huu utakuwa na ushindani mkubwa ukilinganisha na uliopita kutokana na karibu kila timu ama kufanya usajili mzuri au kuimarisha mabenchi yao ya ufundi achilia mbali kuwa na udhamini binafsi wa uhakika.
Zoezi la usajili lililomalizika hivi karibuni limeonesha wazi timu kusajili kwa mipango licha ya kuwa zipo timu zilizomaliza mpango huo mapema sana na zingine zikikubali kulimaliza suala hilo katika muda wa nyongeza kwa kukubali kulipa na faini sh. 500,000 kwa kila mchezaji atakayesajiliwa katika muda huo.
Azam na Simba pekee waliokubali kulimaliza zoezi hilo katika muda wa nyongeza baada ya kusajili wachezaji Pape Abdoulaye Ndew na Boniface Maganga (Simba) na Diouf kwa upande wa Azam.
Bila shaka hiyo ilikuwa ni silaha yao ya mwisho kuhakikisha hakuna ‘matobo’ katika usajili wao hivyo timu hizo zitarajiwe kufanya makubwa katika msimu huu wa 2015/2016 ambapo bingwa ataweka kibindoni kitita cha Sh. Mil 75.
Lakini Azam mabingwa wapya wa michuano ya Kombe la Kagame, kupitia michuano hiyo imetosha kabisa kukisuka kikosi chao hivyo kuwa moja kati ya timu zitakazoianza vizuri ligi ya msimu huu japo hiyo haiwezi kuwa uhakika kwani cha msingi pia ni kujipanga na kucheza vizuri karata zake.
Kwa upande wa Yanga wao waliungana na timu zingine zilizosalia kufunga usajili wao katika muda wa awali uliotolewa, hali inayoonesha wazi hawana wasi na vikosi vyao na ndiyo maana waliwahi kumaliza.
Lakini kati ya hao zipo timu zilizofunga mapema usajili wao kutokana na kukabiliwa na ukata kama vile Ndanda na Majimaji hivyo hawakuwa na namna bali kukubaliana na hali kwa kusajili wachezaji mapema kwa bei ya kawaida na wala hawakutaka kujipa presha zaidi kufanya hesabu mapema na kulifunga zoezi hilo.
Uzoefu unaonesha kila wageni wanapoingia katika Ligi Kuu wanaingia wakiwa na ushindani mkubwa, mfano mzuri ni Mbeya city ilipopanda misimu miwili iliyopita ilikuwa katika kiwango kikubwa kiasi cha kutishia uhai wa vigogo vya soka nchini. Hali kadhahalika Ndanda na Stand United msimu uliopita zilifanya vema tu.
Kuna kila dalili African Sports ya Tanga moja kati ya timu zilizowahi kuwika katika miaka ya 80 nayo ikirudi kwa nguvu hivyo kurudisha ile hamasa ya upinzani wa jadi mkoani humo dhidi ya Coastal Union.
Timu kongwe za ligi hiyo kama vile Ruvu JKT, Coastal Union, Mtibwa na Kagera Sugar zinaonekana kutulia huku zikijiandaa kuja na mbinu tofauti kabisa kuhakikisha nazo zinakuwa siyo wasindikizaji tu bali kushika nafasi za juu na kupata tiketi ya kushiriki michuano ya kimataifa.
Lakini pia uwepo wa timu nyingi zenye udhamini binafsi mbali na ule wa Vodacom au Azam Televisheni utasaidia sana kuifanya ligi hiyo kuwa na ushindani kwani sasa wachezaji wa timu husika watakuwa na uhakika wa malipo yao hali itakayowafanya kupigana kufa na kupona.
Stand United chini ya udhamini mnono wa Bilioni …..kutoka  kampuni ya madini ya Acacia utaifanya timu hiyo msimu huu kuja kivingine tofauti na changamoto iliyokutana nazo msimu uliopita timu kukabiliwa na ukata kiasi cha baadhi ya wachezaji kuikimbia timu.
Mwadui ya Shinyanga nayo ikiwa chini ya kampuni ya Madini pia ikiwa na kocha mwenye mbwembwe na maneno mengi bila shaka licha ya ushindani vilevile kuwa chini ya kocha mwenye kuifahamu ligi hiyo kutaibeba timu hiyo.
Mbeya City pengine inaweza kuja kivingine hasa kutokana na kuondokewa na wachezaji wake kadhaa tegemeo kutaifanya kuchukua muda katika kukijenga kikosi.
Lakini pia uzoefu wa wachezaji waliobaki pamoja na kocha wao Juma mwambusi unaweza kuleta maajabu kama ilivyofanya simu wa kwanza ilipopanda Ligi Kuu kwa kuzichachafya timu vigogo na hatimaye kushika nafasi ya tatu.
Kilio kikubwa cha waamuzi kimefanyiwa kazi kwa Bodi ya Ligi kuweka kanuni mpya zinazowafanya sasa kutumia ushahidi wa picha za televisheni kuwahukumu waamuzi watakaokwenda kinyume na kazi yao.
Ili kuipa hadhi ligi hiyo pamoja na kuipandisha chati kuifanya kuwa moja kati ya Ligi bora barani Afrika suala la uamuzi ni nyeti na linalopaswa kuangaliwa kwa jicho la tatu.
Lakini uzingatiwaji wa kanuni na sheria za mashindano, bodi ya ligi na TFF kwa ujumla ndiyo silaya kubwa itakayotoa taswira na ubora wa michuano hiyo katika kufikia kumpata bingwa sahihi.
Mechi za ufunguzi zitatoa mwanga fulani hata kama kama bado ligi itakuwa change. Mechi hizo ni Yanga na Coastal Union, Ndanda na Mgambo, African Sports dhidi ya Simba, Stand na Mtibwa, Azam dhidi ya Prisons, Mbeya City ikipambana na Kagera na Majimaji ikimenyana na Ruvu JKT.   
Kuanza kwa Ligi hiyo kutatoa picha ya timu zipi zilitumia msimu mrefu wa usajili kwa manufaa ya klabu. Timu iliyojiandaa vema bila shaka ndiyo itakayofanya vizuri msimu huuu kama si kutwaa ubingwa.

Imeandaliwa na Asha Muhaji.


No comments

Powered by Blogger.